²Ù±ÆÊÓƵapp

Redirecting...

²Ù±ÆÊÓƵapp

The Africa Renewal website has relocated to:

You are being redirected automatically. If not, click the link above.

COP26 hadi COP27: Kusonga kutoka kwa 'fursa bora ya mwisho' hadi 'kuchukua fursa'

Get monthly
e-newsletter

COP26 hadi COP27: Kusonga kutoka kwa 'fursa bora ya mwisho' hadi 'kuchukua fursa'

Njia tano za kusaidia Afrika kujiandaa na kuchochea hatua katika COP27
Afrika Upya: 
6 December 2021
Vijana waandamana kwa ajili ya hatua za hali ya hewa kabla ya COP26.
Gettyimages/ Leo Patrizi
Vijana waandamana kwa ajili ya hatua za hali ya hewa kabla ya COP26.
Ikiwa huwezi kusoma sasa, sikiliza tu toleo la sauti: 

Kabla ya wajumbe kutoka sehemu mbalimbali za dunia kukusanyika Glasgow, Scotland, mwezi Novemba kwa ajili ya kongamano la 26 la Umoja wa Mataifa la Mabadiliko ya Hali ya Hewa, (COP26), tukio hilo lilikuwa likiitwa ‘fursa bora ya mwisho’ ya kutatua mabadiliko ya hali ya hewa. 

Tukitathmini Mkataba wa Hali ya Hewa wa Glasgow kama hatua madhubuti ya mabadiliko, basi tathmini yetu itakuwa ile ya kutofaulu. Hata hivyo, hiyo haimaanishi kuwa yote yamepotea.  Milango fulani imefunguliwa, hata ikiwa bado hatujaipitia.  COP ijayo itafanyika nchini Misri chini ya mwaka mmoja kuanzia sasa.  Hii ndio fursa ambayo lazima tuichukue. Kuna kasi ya kimataifa kuhusu hatua za hali ya hewa, hata ikiwa hatua za kisiasa bado zinalegea.

Ukweli ni kwamba matarajio yalikuwa tayari yamelemazwa, hata kabla ya wajumbe kuwasili Glasgow, kwa sababu katika masuala mawili makuu --hatua kwenye ahadi kupunguza kabisa ongezeko la joto duniani, na fedha za kusaidia uzalishaji wa chini wa kaboni katika mataifa yanayoendelea – maamuzi tayari yalikuwa yametolewa kwa nmna fulani na G20, na wazalishaji wakubwa wa gesi, hata kabla ya beji zozote za mjumbe kuchukuliwa katika Kituo cha Maonyesho cha Scotland kwenye kingo za Mto Clyde.

Licha ha haya yote, hatua kubwa zilifikiwa. 

Ahadi ya kwanza ya kupunguza makaa ya mawe na nishati zingine za visukuku; kutambua hasara na uharibifu; na kuundwa kwa hatua za kiufundi kuushughulikia; urudufishaji wa fedha za ukabilifu; ahadi ya kukomesha ukataji miti; na kukamilishwa kwa kitabu cha sheria kuhusu Kifungu cha 6 cha kuwezesha biashara ya kaboni, yote yanawakilisha masuala ya kiufundi ya kudumu yaliyosongeshwa mbele kwa sasa.

Hata hivyo, maendeleo haya ya kiufundi hayawi hatua ya mabadiliko ya hali ya hewa.  Ahadi za Glasgow bado zinatuweka kwenye nafasi bora kwa ongezeko la joto kwa digrii 2.4.  Tathmini ya hivi punde kuhusu ufadhili ilionyesha pengo linaloendelea la dola bilioni 20 kwa mwaka kufikia lengo la dola bilioni 100 la ufadhili wa mabadiliko ya hali ya hewa.

Na kwa nchi za Afrika, zaidi ya digrii 2 za ongezeko la joto linamaanisha hasara ya Pato la Taifa la karibu 5% kwa mwaka ifikapo 2030, kulingana na uchambuzi wa Kituo cha Sera ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa barani Afrika. 

Glasgow ilithibitisha tena ugumu wa kupiga hatua kwenye masuala ya fedha, na ukweli ni kwamba ahadi ya dola bilioni 100 ambayo haijatekelezwa inawakilisha 0.4% tu ya jumla ya fedha za kimataifa zilizochangishwa kukabiliana na janga la COVID-19 katika muda wa chini ya miaka 2. 

Sababu kubwa ya kukata tamaa baada ya Glasgow ni kwamba rekodi ya utekelezaji iko chini sana.  Mkataba wa Paris hatimaye umejengwa kwenye ahadi za mataifa binafsi.  Ahadi hizi hazijatimizwa.  Kwa hivyo, huku ahadi za Glasgow zikiwa hazijatimizwa, swali ni: je, ahadi hizi ambazo hata hazitoshelezi zitatekelezwa?

Kuwekeza katika miradi inayohusiana na ukabilifu katika sekta muhimu kama vile kilimo kunaweza kuleta faida kubwa kwenye uwekezaji katika uongezaji wa thamani na uundaji wa nafasi za kazi.

  • Nchini Afrika Kusini, faida ya zaidi ya asilimia 150 inaweza kupatikana kwa matengenezo na uwekezaji katika mbuga, huku kilimo cha misitu na mipango ya upandaji miti kuleta faida ya zaidi ya asilimia 100.
  • Katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, faida ya kufikiai asilimia 450 inawezekana kwa kuwekeza katika kilimo cha unyunyiziaji maji na hatua zinazohusiana na kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa.
  • Nchini Kenya, faida ya zaidi ya asilimia 200 inawezekana kutokana na matumizi ya mbegu zinazostahimili katika kilimo na faida kama hiyo pia inaweza kupatikana kwa matengenezo na kuwekeza katika mbuga za asili.

Mtazamo wa kupoteza matumaini ni chombo muhimu cha kuunda hatua halisi.  Kwa hiyo, licha ya mapungufu ya COP26, ambayo ni sehemu ya mapambano ya ushirikiano wa mataifa mengi, hapa kuna masuala matano muhimu yanayoweza kutusaidia kujiandaa kwa ajili ya COP27 yenye lengo la kujenga hatua za vitendo vya kuhimili mabadiliko ya hali ya hewa kwa nchi za Afrika:

1. Kwa usaidizi sahihi Afrika inaweza kuleta ufufuo wa kijani

Ukuaji wa Afrika na maendeleo ya kupendeza mwanzoni mwa karne hii ulijengwa kwenye mauzo ya bidhaa na fursa mpya za biashara za kimataifa. Hata hivyo, ukuaji huu haujajenga mifumo ya thamani endelevu na inayostahimili, na marekebisho ya haraka yanahitajika kwa Afrika ili kuepuka kupoteza mwongo mwingine. 

Uchanganuzi wa Tume ya Uchumi ya Umoja wa Mataifa kwa Afrika (ECA) umepata uwiano mkubwa sana katika nafasi za kazi zilizoundwa na uongezaji wa thamani ya jumla katika uchumi kwa kufuata uwekezaji katika sekta za kijani badala ya uwekezaji katika sekta zinazotokana na mafuta.  Faida ya uwekezaji katika nchi zilizofanyiwa uchunguzi ilionyesha hadi asilimia 420 ya faida bora katika uongezaji wa thamani ya jumla na hadi asilimia 250 ya faida bora katika uundaji wa nafasi za kazi kutokana na uwekezaji katika sekta kama vile nishati mbadala, kilimo bora kwa hali ya hewa na utalii unaozingatia asili kuliko katika sekta ya nishati ya visukuku. 

Kwenye nishati mbadala, nchi zote za Afrika ni muhimu kama fursa za uwekezaji katika utoaji wa nishati mbadala - huku nchi 24 kati ya 54 zikiwa na chini ya nusu ya jumla ya watu walio na umeme - pamoja na wahusika muhimu katika mfumo wa thamani na madini mengi muhimu kwa teknolojia ya betri inayopatikana barani.  

Hakutakuwa na ufufuaji wa kijani duniani kama Afrika si sehemu ya mfuko wa uwekezaji.

2. Ufadhili wa kimbele ni muhimu

Nchi za Afrika zinahitaji njia za kuaminika za ufadhili ili kuweza kuwekeza mapema ili kuongeza faida kwenye uwekezaji.  Kama ilivyotambuliwa kwenyea utafiti wa kimataifa kutoka kwa Nick Stern mwaka wa 2020, uzalishaji uko juu kama uwekezaji ukifanywa mapema. 

Uchanganuzi wa ECA pia unaonyesha kuwa Afrika inaweza kuwa imepoteza hadi asilimia 5 ya ukuaji kutokana na kucheleweshwa kwa uwekezaji wa mwanzo katika mwaka wa 2020. 

Kuelekeza uwekezaji katika maeneo kama vile nishati safi na miundomsingi ya usafiri ni vizalishaji vya kiuchumi na vinaweza kuleta mzunguko mzuri wa uwekezaji.

Nchi za Afrika zinategemea sana ufadhili kutoka nje - zinazotoka kwa wafadhili au kutoka kwa uwekezaji wa moja kwa moja wa kigeni.  Ukosefu wa ukuaji wa masoko ya mitaji ya ndani ya nchi unamaanisha kuwa hali hii inaweza kuendelea, ingawa ufadhili wa kimkakati mwanzoni katika sekta zinazofaa unaweza kuleta mabadiliko. 

Katika lengo la jumla la fedha za kimataifa, wapatanishi wa Afrika walitoa wito kwa lengo la kila mwaka la dola bilioni 700 huko Glasgow. 

Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) inakadiria kuwa michango ya kitaifa ya nchi za Afrika (NDCs) itawakilisha fursa ya uwekezaji ya zaidi ya dola trilioni 3 ifikapo 2030.  Huenda ikafaa kuwa na lengo mahususi zaidi ambalo ni mahususi kwa kiasi cha fedha kinapaswa kupatikana kama ruzuku na mikopo ya muda mfupi na malengo badilifu (ambayo hayafai kuwekewa kikomo) kwa malengo ya kifedha ya kibinafsi. 

Hili ni muhimu hasa huku mazungumzo kuhusu utoaji wa Haki za Fedha Maalum (SDRs) yanazidi kushika kasi, kwa kuwa kutoa hela zinazostahili kwa Afrika na mataifa mengine yanayoendelea kutakuwa muhimu katika kukabiliana na COVI9-19 na kustahimili mabadiliko ya hali ya hewa.

Kwa Afrika, kuwa na uwezo wa kutoa ufadhili wa sekta binafsi wa mabadiliko ya hali ya hewa kutategemea usaidizi sahihi wa mbeleni -- iwe kwa kuunganishwa au dhamana. 

Kwa vyovyote vile, Afrika kwa sasa iko nyuma katika upatikanaji wa fedha za mabadiliko ya hali ya hewa kutoka sekta binafsi, na kuvutia chini ya asilimia 3 ya fedha za mabadiliko ya hali ya hewa za sekta binafsi duniani. 

Afrika na Mashariki ya Kati kwa pamoja pia hutoa chini ya asilimia 1 ya jumla ya idadi ya dhamana kwa kijani duniani kote. Kufungua zaidi masoko ya dhamana za kijani na majini kutakuwa hatua muhimu kwa Afrika.

3.  Nishati ya Afrika ni ufunguo wa kufungua ukuaji

Kwa upande wa uzuiaji, Afrika tayari iko upande mzuri kwa ina 17% ya jumla ya watu ulimwenguni huku ikichangia chini ya asilimia 4 ya uzalishaji wa gesi chafu duniani.

Kulingana na teknolojia zinazopatikana kwa sasa, na kuhusu demografia ya Afrika, uzalishaji wa gesi chafu barani ni lazima utaongezeka. 

Hii ndiyo sababu Mkataba wa Paris unatambua kuwa nchi zinazoendelea zitachukua muda mrefu zaidi kufikia kiwango cha juu cha uzalishaji wa gesi chafu kuliko nchi zilizostawi, ambazo lazima zitekeleze sehemu yao ya uzuiaji ili kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa. 

Ustahimilivu wa Afrika utafikiwa vyema zaidi kwa kutumia njia za nishati mbadala na kuendeleza mifumo ya thamani ya kitaifa na kikanda katika utengenezaji na usambazaji wa teknolojia kama hizo. 

Kwa kiwango kikubwa, Afrika imeathiriwa katika miaka ya hivi karibuni na kushuka kwa bei ya mafuta -- nchi zinazozalisha na waagizaji.  Uwekezaji madhubuti wa muda mrefu katika nishati safi unaweza kuzuia hatari hizi na kuwezesha gharama zinazotabirika zaidi za kufanya biashara.  Hii ni muhimu kwa ukuaji wa viwanda wa bara hili na kufungua zaidi uwezo wa Biashara Ndogondogo (MSMEs).

Mpito wa haki kwa Afrika pia utahitaji kutambuliwa kuwa uzalishaji ziada utahitajika kwa ajili ya kuongeza uwekezaji kwa haraka kwa nishati safi. Kwa mfano, ikiwa Afrika ilifaa kuongeza uzalishaji wake wa umeme mara dufu kwa kutumia gesi asilia pekee, hiyo ingewezesha kuzidisha uwekezaji wa nishati ya jua na upepo kwa mara 38, huku kukiwa na ongezeko la asilimia 1 tu ya uzalishaji wa gesi chafu duniani.

kutoa ufadhili wa kusaidia mpito kutoka kwa kutumia makaa ya mawe pia unaweza kutoa mfano wa mfumo unaoweza kuigwa katika nchi nyingine, wa jinsi ya kutumia usaidizi kutoka nje kuelekeza upya sekta ya nishati na kuepuka kunaswa katika 'mali iliyokwama'.

4.  Ustahimilivu kupitia ukabilifu ni muhimu kwa ustawi wa kiuchumi

Ukabilifu huu hutengewa rasilimali chache za mapambano dhidi ya mabadiliko ya hali ya hewa, hivyo basi ahadi za huko Glasgow kuongeza ufadhili mara dufu wa kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa. 

Uwekezaji wa kimbele wa kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa hupunguza gharama za muda mrefu za uwekezaji. Kama inavyoonyeshwa katika Kituo cha Ukabilifu cha Kilimwengucha 2021 Ripoti ya Hali na Mwekeleo, gharama ya hatua za ukabilifu kupitia kilimo inakadiriwa kuwa dola bilioni 15 kwa mwaka, ambayo inawakilisha chini ya asilimia 10 ya makadirio ya dola bilioni 201 ya gharama ya kila mwaka ya kulipia misaada baada ya mafuriko, ukame, na majanga kama hayo ya kimazingira.

Uchunguzi uliofanywa na ECA, ambao unaangaziwa katika ripoti hiyo unaonyesha wazi kuwa kuwekeza katika miradi inayohusiana na ukabilifu inayohusishwa na sekta muhimu kama vile kilimo kunaweza kuleta faida kubwa kwenye uwekezaji katika uongezaji wa thamani katika uchumi na uundaji wa nafasi za kazi.

  • Nchini Afrika Kusini, faida ya zaidi ya asilimia 150 inaweza kupatikana kwa ukarabati na uwekezaji katika mbuga, huku kilimo cha misitu na mipango ya upandaji miti kuleta faida ya zaidi ya asilimia 100.
  • Katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, faida ya kufikia asilimia 450 inawezekana kwa kuwekeza katika kilimo cha unyunyiziaji maji na hatua zinazohusiana na kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa.
  • Nchini Kenya, faida ya zaidi ya asilimia 200 inawezekana kutokana na matumizi ya mbegu zinazostahimili katika kilimo na faida kama hiyo pia inaweza kupatikana kwa matengenezo na kuwekeza katika mbuga za asili.

5.  Afrika inapaswa kutuzwa kwa kutozalisha gesi chafu kwa wingi

COP26 pia ilihitimisha mazungumzo ya biashara ya kaboni chini ya Kifungu cha 6 cha Mkataba wa Paris.  Ingawa kuna mashaka yanayotolewa kuhusu kutotimizwa kunakoweza kutokea, kwa kuzingatia ukosefu wa usahihi katika baadhi ya fafanuzi, nchi za Afrika zina fursa nzuri mbele ya COP27 ya kutumia mali zao za asili za kuweza kuimarisha uwezo wa kustahimili kwa kulinda maeneo muhimu, huku zikiongeza mtaji unaohitajika sana ambao unaweza kuwekezwa katika vipaumbele vya kitaifa. 

Ardhi zenye mashimo za Bonde la Kongo pekee ni sawa na thamani ya miaka mitatu ya uzalishaji wa hewa chafu duniani. 

Wakati huohuo, nyasi za bahari na mikoko ambayo hupatikana katika Bahari ya Atlantiki ya Afrika na mwambao wa Bahari ya Hindi imethibitishwa kuwekewa masharti kutokana na kaboni mara 2-3 zaidi ya misitu ya mvua ya kitropiki. 

Mpito wa haki kwa Afrika pia utahitaji kutambuliwa kuwa uzalishaji zaidi utahitajika kwa ajili ya kuongeza uwekezaji kwa haraka kwa nishati safi." "Kwa mfano, ikiwa Afrika ilifaa kuongeza uzalishaji wake wa umeme mara dufu kwa kutumia gesi asilia pekee, hiyo ingewezesha kuzidisha uwekezaji wa nishati ya jua na upepo kwa mara 38, huku kukiwa na ongezeko la asilimia 1 tu ya uzalishaji wa gesi chafu duniani.
Bw. Jean-Paul Adam
Mtaalamu wa mabadiliko ya hali ya hewa katika UNECA

Shaka ni kwamba huku Afrika ikiwa na baadhi ya misitu mingi iliyosalia, pia ina kasi kubwa ya ukataji miti ikilinganishwa na mabara mengine.  Kwa hivyo, bila uangalifu na umakinifu, njia ya kaboni ya Afrika inaweza kuwa vyanzo vya uchafuzi. 

Cha umuhimu ni kuwekeza katika kulinda njia hizi za kaboni na huku kunaweza pia kuleta fursa endelevu za kutafuta riziki. 

Programu ya upandaji miti ya Urithi wa Kijani wa Ethiopia ni mfano wa kuvutia wa jinsi matengenezo ya mazingira, yanaolenga kupunguza mmomonyoko wa udongo na athari za mafuriko, yanaweza pia kutumika kuzalisha njia za kutafuta riziki. Kwa mfano, kupanda miti ya matunda ambayo italeta faida kwa jamii, huku ikishughulikia mahitaji ya nishati, na kupunguza shinikizo la ukataji miti kwa ajili ya kuni na kuunda fursa mpya za kuongeza thamani. 

Gabon pia ina hamu kubwa katika kupendekeza kuongeza thamani zaidi kwa rasilimali zake endelevu za mbao, kutoa ulinzi kwa misitu huku pia ikiongeza njia za kutafuta riziki kwa jamii.

Tathmini zilizofanywa na ECA kwa ushirikiano na Dalberg zimeonyesha uwezekano wa mtiririko wa kifedha wa dola bilioni 15-30 na bei za kaboni zikiwiana na malengo ya Mkataba wa Paris. 

Nchi kadhaa za Afrika pia zimezungumza baada ya COP26 kuhusu hamu ya kukuza soko la kaboni barani Afrika, kuruhusu nchi za Afrika kutumia mitaji yao ya asili na kutumia faidia zake katika ukabilifu na ustahimilivu wa mabadiliko ya hali ya hewa.

Kwa kuhutimisha, makabilio ya COVID-19, na yale ya COP26 yamesisitiza vikwazo vya mtazamo unaohusisha mataifa mengi. Tunakwazwa kwa ukosefu wa nia njema ya kisiasa, na tunalazimishwa kwenda kwa kasi ya mataifa kaidi zaidi. 

Katika kukabiliana na COVID-19 na mabadiliko ya hali ya hewa, ushirikiano unaohisisha mataifa mengi umeimarisha ukosefu wa usawa wa nafasi ya maendeleo ya kimataifa. 

Katika kukabiliana na janga la COVID-19, nchi za G20 zimechangisha zaidi ya dola 11,000 kwa kila mtu katika harakati hizo, huku kwa nchi za mapato ya chini matumizi kwa kila mtu ni wastani wa dola 57 pekee.  Katika nchi moja ya Afrika matumizi ni dola 11 pekee kwa kila mtu. 

Maelewano ya Glasgow yamekuwa kudumisha uwazi, na kuhakikisha kuwa mtazamo unaohusisha mataifa mengi unazidi kufaa, hata ikiwa ni wa polepole sana kukidhi udharura halisi unaoletwa na janga la hali ya hewa.

Nchi za Afrika zinapaswa kupongezwa kwa nia yao ya kuendelea, hata wakati ambapo ufadhili kutoka nje haujapatikana. 

ni kielelezo cha taasisi hii ya nchi za Afrika katika kuandaa ukabilifu thabiti.

Ili kuchochea hatua halisi katika COP27, lazima tulenge kujijenga wenyewe kindani kama nchi za Afrika. 

Bw. Adam ni Mkurugenzi, Idara ya Teknolojia, Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Maliasili (TCND) wa Tume ya Uchumi ya Umoja wa Mataifa kuhusu Afrika (UNECA). Hapo awali aliwahi kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Fedha wa Ushelisheli.

More from this author